IKIWA ni siku mbili zimepita tangu tasnia ya muziki wa taarabu
hapa nchini kumpoteza mkurugenzi, mtunzi na mpiga kinanda mahiri wa
kundi la East African Melody, Haji Mohamed, mchana wa jana imepata pigo
tena la kumpoteza nguli mwingine, Fatuma Baraka ‘Bi. Kidude’.
Akizungumzia kifo cha nguli huyo, mwanae Abdallah Baraka alisema
marehemu mama yake alikuwa akisumbuliwa na ugonjwa wa kisukari kwa muda
mrefu hadi umauti unapomkuta akiwa nyumbani kwake Bububu mjini
Zanzibar.
Baraka alisema mama yake siku kadhaa zilizopita hali yake haikuwa
shwari na kuwalazimu kumpeleka hospitalini mara kwa mara kwa ajili ya
kuangalia afya yake ambayo ilikuwa ikiwapa wasiwasi hadi jana majira ya
saa 7 mchana umauti ulipomkuta.
“Mama yangu alikuwa anasumbuliwa na kisukari kwa muda mrefu, ila siku
za hivi karibuni hali yake haikuwa nzuri na kumkimbiza hospitalini
mara kwa mara ili kupata matibabu, lakini imeshindikana kwani Mungu
amependa zaidi,” alisema Baraka na kuongeza kuwa marehemu atazikwa leo
saa 7 mchana katika makaburi ya Kitumba visiwani humo.
Bi. Kidude alikuwa gwiji wa muziki huo na kutamba barani Afrika na
nje kutokana na umahiri wake wa kutumbuiza jukwaani vibao vyake
mbalimbali kikiwamo ‘Muhogo wa Jang’ombe’.
Muziki huo ambao ni mchanganyiko wa muziki toka nchi za Kiarabu na
vionjo vya muziki wa Kiafrika, umejikita sana katika mwambao wa pwani
ya Afrika Mashariki.
Bi. Kidude alizaliwa Kijiji cha Mfagimarigo Unguja katika familia ya
watoto saba, ambako baba yake Mzee Baraka alikuwa ni mfanyabiashara wa
nazi, zao ambalo ni la kutumainiwa Zanzibar.
Bi. Kidude aliwahi kusimulia kuwa hafahamu tarehe halisi aliyozaliwa,
isipokuwa anachojua ni kwamba alizaliwa wakati rupia ikitumika kama
fedha. Wataalamu wa mahesabu baada ya kupata taarifa hizo wakampigia
mahesabu na kumkabidhi miaka yake kwamba ni zaidi ya miaka 100.
Katika historia yake enzi za uhai wake, Bi. Kidude alisema uimbaji
aliuanza tangu alipokuwa na miaka 10 na alijifunza kutoka kwa msanii
mkongwe na aliyetamba sana enzi hizo, Sitti binti Saad.
Anasema wageni wengi kutoka sehemu mbalimbali walikuwa wakifika
Zanzibar kumwona Sitti, na kwa vile walikuwa wako karibu, basi alikuwa
akiwapeleka wageni wale nyumbani kwake, na wakifika huko walikuwa
wakiingia ndani na yeye kubakia nje.
Huko ndani, Bi. Sitti alikuwa akiwaimbia wale wageni na yeye akiwa
nje akimsikiliza kwa makini, akimuigiza jinsi alivyokuwa akiimba na
kutumia nafasi hiyo ambayo ilimfanya kupata umaarufu zaidi hadi akawa
mahiri sana katika uimbaji.
Alipokuwa na miaka 13, kwa mara ya kwanza alitoroka nyumbani kwao
Zanzibar na kukimbilia Tanzania Bara, baada ya kulazimishwa kuolewa.
Lakini alipokuwa kigoli wa kutosha kuolewa, aliolewa ingawa ndoa hiyo
nayo haikudumu kutokana na manyanyaso aliyokuwa akiyapata, hivyo
aliamua kukimbilia kaskazini mwa Misri ikiwa ni katika miaka ya 1930,
ambako huko aling'ara sana katika fani yake ya uimbaji na uchezaji
ngoma.
Lakini ilipofika miaka ya 1940, aliamua kurudi nyumbani Zanzibar ambako aliendelea na shughuli zake za uimbaji.
Bi. Kidude enzi zake, alikuwa hategemei kazi moja tu ya kuimba, kwani
pia ni mfanyabiashara ya wanja na hina ambavyo anavitengeneza yeye
mwenyewe. Pia ni mtaalamu wa matibabu kwa dawa za miti shamba na zaidi
ya hayo ni mwalimu mzuri sana wa unyago na alianzisha chuo chake
mwenyewe na anasema katika wanafunzi wake wote, hakuna aliyepata talaka
kutoka kwa mumewe.

Post a Comment